Suala la ardhi katika riwaya teule za kiswahili: Tathmini ya kovu moyoni na kufa kuzikana
Date
2018
Authors
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Chuka University
Abstract
Ardhi ni mojawapo ya rasilimali muhimu katika maisha ya mwanadamu. Suala la rasilimali ya ardhi ulimwenguni hasa nchini Kenya limekuwa nyeti na kuibua mijadala ya kijamii na kiakademia tangu enzi za ukoloni na hata baada ya uhuru. Utafiti huu ulikusudia kuchunguza jinsi suala la ardhi limesawiriwa na waandishi wa riwaya teule za Kiswahili. Riwaya zilizohakikiwa ni Kufa Kuzikana (Walibora, 2003) na Kovu Moyoni (Habwe, 2014). Msisitizo ulikuwa kuangazia jinsi wasanii wa riwaya hizi walivyoangazia migogoro kuhusu ardhi kuonyesha matatizo yaliyotokana na mikinzano kuhusu rasilimali hiyo pamoja na athari zake. Hii ni kwa msingi kuwa fasihi ni mojawapo ya nyenzo inayoweza kuchangia kuangazia matatizo yanayokumba jamii yoyote iwayo. Aidha, ni chombo muhimu cha kuelimisha, kuhamasisha na kuzindua jamii pana kuhusu matatizo yake. Madhumuni ya utafiti huu yalikuwa kuchunguza jinsi Walibora na Habwe wametumia fasihi kudhihirisha mizozo ya ardhi kwa kurejelea tungo zao, kuchunguza jinsi ambavyo walitumia fani za lugha kuwasilisha athari za mizozo ya ardhi na kubainisha suluhisho walilolitoa kama wasanii walio katika sehemu ya jamii zilizokumbwa na migogoro ya ardhi. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya Baadaukoloni ambayo inahusishwa na kazi za Cesaire (1950), Fanon (1961) Said (1978) na Bhabha (1994), ambayo ilitumika ili kufafanua jinsi waandishi wa riwaya teule wamedhihirisha athari za ukoloni katika suala la ardhi. Utafiti huu ulitumia uteuzi wa sampuli wa kimakusudi kama njia ya kutathmini riwaya teule. Data ilipatikana kutoka kwenye matini iliyoteuliwa kimakusudi. Mtafiti alisoma riwaya husika kwa kina na kubaini maneno na mafungu ya maneno yaliyohusiana na suala la ardhi. Aidha, mtafiti alihakiki na kuchunguza jinsi wasanii wa riwaya za Kufa Kuzikana na Kovu Moyoni wamefafanua matatizo ya ardhi pamoja na suluhisho wanazotoa. Uchanganuzi wa kimaelezo wa data ulifanywa na kuwasilishwa kwa maandishi ya kinadhari. Ilibainika kuwa wasanii wa riwaya teule wamerejelea suala la ardhi nchini Kenya kama tatizo la jamii ambamo riwaya hizo ziliibuka huku wakiwasawiri Wakenya kama wahusika katika kazi zao kwa mujibu wa vipindi mbalimbali vya kihistoria. Vilevile, wameangazia mambo mbalimbali ambayo yanaweza kutumika ili kusuluhisha matatizo ya ardhi nchini. Utafiti huu utawanufaisha wahakiki wa fasihi katika kushadidia mtazamo kwamba, fasihi inaakisi kikamilifu matatizo yanayoibuka katika jamii ilimoibuka. Kwa hivyo, ni chombo madhubuti kinachoweza kutumiwa kutatua matatizo hayo
Description
library@chuka.ac.ke
www.chuka.ac.ke
Keywords
Rasilimali ya ardhi, Migogoro ya ardhi, Mizozo ya kijamii, Riwaya za Kiswahili, Kufa Kuzikana, Kovu Moyoni, Ken Walibora, John Habwe, Ukoloni na ardhi, Athari za ukoloni, Nadharia ya baadaukoloni, Migogoro ya kihistoria, Fasihi na jamii, Suluhisho la migogoro ya ardhi, Uhakiki wa kifasihi, Fasihi na mabadiliko ya kijamii, Matumizi ya fani za lugha, Migogoro ya kihistoria nchini Kenya, Mikakati ya uhakiki wa kijamii, Uwakilishi wa jamii katika fasihi